Mwanafunzi Julius Isingoma ameelezea jinsi alivyonusurika kimuujiza wakati wa shambulio la usiku na watu wanaoshukiwa kuwa waasi wa Kiislamu kwenye bweni lake la shule magharibi mwa Uganda.
“Nilipaka damu za wenzangu waliofariki dunia mdomoni, masikioni na kichwani ili washambuliaji wafikiri nimekufa,” alisema alipokuwa katika Hospitali Kuu ya Bwera wilayani Kasese.
Takriban watu 40 - 37 kati yao wakiwa wanafunzi - walikufa katika shambulio la shule ya sekondari katika mji mdogo wa Mpondwe Ijumaa usiku.
Rais wa Uganda Yoweri Museveni alilaumu shambulio hilo dhidi ya Allied Democratic Forces (ADF), akiongeza kuwa "kuna uwezekano walishirikiana na wahalifu wengine kwa sababu nasikia shule ilikua na mizozo". Hakufafanua zaidi, lakini aliapa kuwasaka wanamgambo hao katika maficho yao katika mpaka wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.
Hata hivyo, ADF bado haijatoa maoni. Iliundwa katika miaka ya 1990 na kutwaa silaha dhidi ya Bw Museveni, kwa madai ya kuteswa kwa Waislamu walioachia.
Kiongozi wake aliripotiwa kuahidi utiifu kwa kundi la Islamic State (IS) mnamo 2016.
Lakini haikuwa hadi Aprili 2019 ambapo IS ilikubali kwa mara ya kwanza shughuli zake katika eneo hilo, ilipodai kushambulia maeneo ya jeshi karibu na mpaka na Uganda.
Taarifa hii iliashiria tangazo la IS "Mkoa wa Afrika ya Kati" (Iscap).
Wanafunzi sita wanaaminika kutekwa nyara huku wanamgambo hao wakirejea DR Congo.
Julius alikuwa miongoni mwa watu sita waliofanikiwa kunusurika katika shambulio hilo lililodumu kwa saa kadhaa.
Hawakuwatambua washambuliaji, lakini alisema walikuwa watu wenye bunduki ambao walianzisha mashambulizi yao mwendo wa saa 22:00 kwa saa huko.
Walifika bweni la wavulana lakini wanafunzi walikuwa wamefunga baada ya kugundua walikuwa hatarini.
"Waliposhindwa kufungua mlango walirusha bomu ndani ya bweni kisha kutumia nyundo na shoka kuvunja mlango," alisema.
Julius alikuwa amesimama nyuma ya wanafunzi wengi waliokuwa wametengeneza ngao karibu na mlango na kuuawa kwa kupigwa risasi wakati wanamgambo hao walipoingia bwenini.
Kulikuwa na vilio vya wanafunzi wakipigwa risasi, kukatwa au kupigwa risasi hadi kufa.
Harakaharaka akapanda juu ya kitanda cha darini, akatoa baadhi ya mbao za dari, na kuruka ndani kujificha.
Kutoka hapo akiwa hoi akawatazama wenzake wakiuawa kikatili na wale wauaji kisha wakachoma magodoro na kuondoka zao.
"Nilizidiwa na moshi huo na nikashuka tena ndani ya bweni kwa kishindo," alisema.
Wanamgambo hao walisikia kishindo hicho na kurudi.
Ni wakati huo Julius alijua lazima atoke kwenye shambulio hilo akiwa hai.
“Nilijilaza karibu na miili ya marafiki zangu iliyokuwa na damu nikiwaza harakaharaka, kisha nikajipaka damu nyingi masikioni na, mdomoni na kichwani na wapiganaji hao walipofika walinichunguza mkono wangu kuona kama kuna mapigo ya moyo na kuondoka zao,” Julius anasema.
Mwingine aliyenusurika, Godwin Mumbere, alikuwa katika bweni moja na Julius.
Kijana huyo mwenye umri wa miaka 18 alikumbana na washambuliaji hao wakienda kwenye bweni la wasichana , na kuwatoa nje na kuwakata kwa mapanga hadi kuwaua.
Kisha wakafika kwenye bweni la wavulana, wakavunja mlango na kuanza kuwashambulia wanafunzi.
Kitanda alichokuwa amejificha Godwin kilipinduliwa na marafiki zake waliokuwa juu walianguka chini na kuuawa.
"Washambuliaji waliniona lakini walidhani nimekufa," aliambia alisema
“Lakini walitoka na kurudi ndani ya bweni ili kuhakikisha kila mtu amekufa.”
"Ni wakati huu ambapo walinipiga risasi mkononi na kuteketeza bweni," alisema.
Godwin alirudishiwa ukweli na kelele za mwanafunzi mwingine aliyesema wanakufa.
Alikimbia nje ya bweni, akapanda lango la shule na kukimbilia kwenye duka la vifaa vya jirani kupitia shamba la kakao. Alifika kwenye nyumba ya kulala wageni na kujificha chini ya gari hadi alipookolewa.
Clarice Bwambare, msimamizi wa Hospitali Kuu ya Bwera, alisema kuwa walianza kupokea miili ya wanafunzi na wakaazi mwendo wa saa 01:00 - takriban saa tatu baada ya shambulio hilo kuanza usiku.
Alibainisha kuwa kati ya miili 20 waliyopokea, 18 ni ya wanafunzi.
Watu watano walionusurika wanaendelea kupata nafuu katika hospitali hiyo. Mmoja wao ni msichana ambaye yuko katika hali mbaya katika chumba cha wagonjwa mahututi. Daktari wa upasuaji alishauri kwamba hawezi kusogezwa kwa sababu ya jeraha kali la kichwa kwa kupigwa na nyundo na waasi.
Bwambare alisema ni mwili mmoja tu ambao haujadaiwa kutoka katika chumba cha kuhifadhia maiti.
Siku ya Jumapili, familia zilizokumbwa na huzuni zilizika wanafunzi 21, kulingana na gazeti la New Vision la Uganda.
Akiwa amelala kwenye kitanda chake cha hospitali, Julius alionyesha majuto kwamba hangeweza kuhudhuria mazishi yao. Alisema anatamani angekuwajeshi ambaye angeweza kuokoa maisha ya marafiki na wafanyakazi wenzake.
Chanzo: bbc.com

FOLLOW US HERE